Yanga Yaunda Kikosi Kazi cha Misheni ya Makombe

Yanga Yaunda Kikosi Kazi cha Misheni ya Makombe

Klabu ya Yanga SC imeanza rasmi maandalizi ya msimu mpya wa mashindano ya kitaifa na kimataifa kwa kuchukua hatua za kipekee ili kuhakikisha inaendelea kuwa kinara. Rais wa klabu hiyo, Injinia Hersi Said, ameunda kikosi kazi maalum kinacholenga kutetea mataji yote ya ndani na kufika mbali zaidi katika michuano ya Ligi ya Mabingwa Afrika. Hii ni sehemu ya mpango mkakati wa Yanga kujiimarisha zaidi kwenye medani ya soka Afrika na duniani.

Yanga Yaunda Kikosi Kazi cha Misheni ya Makombe

Uundwaji wa Kamati Mpya ya Mashindano

Katika jitihada za kuhakikisha mafanikio ya timu yanaimarika, Injinia Hersi ameunda kamati mpya ya mashindano yenye wajumbe nane, ikiwa ni mchanganyiko wa viongozi waliowahi kuleta mafanikio makubwa kwa klabu na sura mpya zenye nguvu.

Hersi amemrudisha Rodgers Gumbo kama Mwenyekiti wa kamati hiyo, mtu ambaye amekuwa na rekodi bora katika usimamizi wa mashindano ya klabu. Gumbo alikuwa kiongozi wakati Yanga ilipochukua mataji makubwa ndani na kufanya vyema kimataifa.

Akiwa na uzoefu wake wa awali, Gumbo anaungwa mkono na Lucas Mashauri, ambaye pia amepewa nafasi ya kuwa makamu mwenyekiti. Mashauri alikuwa na nafasi kubwa katika kuiongoza Yanga kufikia mafanikio ya kuchukua mataji tisa ndani ya misimu mitatu iliyopita.

Wajumbe Wapya Wenye Rekodi Imara

Kamati hiyo mpya inajumuisha vigogo wengine wakubwa, kama Seif Ahmed ‘Seif Magari’ na swahiba wake Davis Mosha.

Wote hawa wawili wamekuwa na mchango mkubwa katika historia ya Yanga, huku Seif Magari akiwa amewahi kuiongoza kamati hiyo wakati wa uongozi wa Yusuf Manji, ambapo timu ilipata mafanikio makubwa.

Mosha, kwa upande wake, aliwahi kuwa makamu mwenyekiti wa Yanga chini ya uongozi wa Imani Madega, jambo ambalo linampa uzoefu mkubwa katika usimamizi wa masuala ya timu.

Wajumbe wengine waliochaguliwa ni pamoja na Pelegrinius Rutayuga, injinia Mustapha Himba, Majid Suleiman, na sura mpya ya Omary Kimosa. Uundwaji wa kikosi kazi hiki unadhihirisha dhamira ya Yanga ya kuhakikisha inaendelea kuwa timu yenye nguvu ndani na nje ya Tanzania.

Mikakati ya Kikosi Kazi

Kikosi kazi hiki kimepewa jukumu la kuhakikisha Yanga inafikia malengo yake ya msimu, yakiwemo kutetea mataji yote ya ndani na kuhakikisha inasonga mbele katika mashindano ya kimataifa.

Taarifa kutoka ndani ya klabu zinaonesha kuwa kamati hii tayari imeanza kufanya kazi kimyakimya, na mojawapo ya majukumu yake ni kuhakikisha maandalizi ya timu kwa michuano ya Ligi ya Mabingwa Afrika yanaenda vizuri.

Yanga imefanikiwa kutinga raundi ya pili ya Ligi ya Mabingwa Afrika baada ya kuwatoa Vital’O ya Burundi. Katika raundi hii, Yanga inakutana na CBE SA ya Ethiopia, ambapo tayari viongozi wa kamati hiyo wameshakwenda nchini Ethiopia kuandaa mazingira ya timu kwa ajili ya mechi hizo muhimu.

Kikosi Kazi Chazamia Ethiopia kwa Misheni ya Makombe

Yanga SC inakabiliwa na mechi muhimu dhidi ya CBE, ambapo wachezaji wake wamegawanyika katika makundi mawili kwa ajili ya safari ya kuelekea nchini Ethiopia. Kundi la kwanza limejumuisha wachezaji waliokuwa kwenye majukumu ya timu ya taifa, huku kundi la pili likiwa ni wachezaji kutoka nchini Ivory Coast wakiongozwa na nyota wa timu, Djigui Diarra, Stephanie Aziz Ki, na Prince Dube. Hii inaonyesha kuwa Yanga imejipanga kikamilifu kuhakikisha inapata matokeo mazuri kwenye mechi hizi za awali.

Tayari Yanga imepeleka timu ya maandalizi mapema nchini Ethiopia ikiongozwa na Mkurugenzi wa Mashindano, Ibrahim Mohammed, ambaye anahakikisha timu inapata mazingira bora ya kufanyia mazoezi kabla ya mechi yao dhidi ya CBE.

Mechi hiyo ya awali inatarajiwa kufanyika katika uwanja wa Abebe Bikila jijini Addis Ababa, Jumamosi hii, na lengo la Yanga ni kuandika historia kwa kufika hatua ya makundi kwa mara ya pili mfululizo katika Ligi ya Mabingwa Afrika.

Mapendekezo ya Mhariri:

  1. Tabora Utd Yalizamisha Jahazi la Kagera Mchana
  2. Fountain Gate Yazindua Dimba la Tanzanite Kwaraa kwa Ushindi Ligi Kuu
  3. Ratiba ya Ligi Kuu Tanzania Bara 2024/2025
  4. Heritier Makambo Ashangazwa na Ubora wa Ligi Kuu
  5. Msimamo NBC Premier league 2024/2025 | Ligi Kuu Bara
Nina uzoefu wa miaka zaidi 6 katika uandishi wa habari nchini Tanzania. Shauku yangu ni kuleta habari muhimu katika nyanja mbalimbali ikiwemo Elimu na Michezo