Taifa Stars Yasafiri Kuelekea Yamoussoukro Kukabiliana na Guinea

Taifa Stars Yasafiri Kuelekea Yamoussoukro Kukabiliana na Guinea

Kikosi cha timu ya taifa ya Tanzania, Taifa Stars, kimeondoka nchini leo kuelekea Yamoussoukro, Ivory Coast, kwa ajili ya kukabiliana na Guinea katika mchezo wa pili wa kuwania kufuzu kwa Fainali za Kombe la Mataifa ya Afrika (AFCON) mwaka 2025.

Mchezo huo muhimu unatarajiwa kupigwa kesho kutwa, huku Stars ikiwa na matumaini makubwa ya kuibuka na ushindi baada ya sare ya 0-0 nyumbani dhidi ya Ethiopia katika mechi yao ya kwanza.

Taifa Stars Yasafiri Kuelekea Yamoussoukro Kukabiliana na Guinea

Maandalizi ya Kikosi na Mafanikio Yanayotarajiwa

Kaimu kocha mkuu wa Taifa Stars, Hemed Suleiman ‘Morocco’, ameeleza kuwa timu imefanya maandalizi ya kutosha, hasa baada ya kufanya tathmini ya mchezo wao dhidi ya Ethiopia. Kwa mujibu wa Morocco, moja ya changamoto kubwa iliyojitokeza katika mchezo wa awali ilikuwa ni ukosefu wa umakini katika umaliziaji wa nafasi za kufunga. Hata hivyo, amesema kuwa wamejikita zaidi kwenye kufanya marekebisho katika eneo hilo na sasa wanajiandaa kikamilifu kwa ajili ya pambano dhidi ya Guinea.

“Kila mmoja wetu yupo tayari kwa changamoto nyingine. Tunaelewa kuwa mechi dhidi ya Guinea haitakuwa rahisi, hasa kwa kuwa wapinzani wetu wamepoteza mchezo wa kwanza. Lakini tumejipanga kupambana na kuhakikisha tunapata alama tatu muhimu ugenini,” alisema Morocco.

Nyota wa Taifa Stars na Maoni Kuhusu Mchezo

Mchezaji wa kiungo, Novatus Dismas, ambaye ameonyesha kiwango bora katika michezo iliyopita, ameongeza kuwa kikosi kimejiandaa kisaikolojia na kimwili kwa pambano hilo, na hawana presha kubwa licha ya changamoto wanazokutana nazo. “Tunajua umuhimu wa mchezo huu, tutapambana kuhakikisha tunapata ushindi kwa ajili ya taifa letu,” alisema Dismas kwa kujiamini.

Guinea Katika Hatua Ngumu

Guinea, ambayo inatumia Uwanja wa Charles Konan Banny uliopo Yamoussoukro kama uwanja wao wa nyumbani baada ya viwanja vyao kukosa vigezo vya CAF, inakabiliwa na shinikizo kubwa kufuatia kushindwa katika mchezo wao wa kwanza dhidi ya DR Congo kwa bao 1-0. Wakiwa bila pointi yoyote, Guinea itahitaji ushindi ili kujiweka kwenye nafasi nzuri ya kusonga mbele katika kundi H.

Hata hivyo, Stars inajivunia rekodi nzuri dhidi ya Guinea, ikiwa mara ya mwisho timu hizo kukutana walitoka sare ya 2-2 katika michuano ya CHAN 2021 iliyofanyika Cameroon. Katika mchezo huo, mabao ya Tanzania yalifungwa na Baraka Majogoro na Edward Manyama.

Msimamo wa Kundi H na Fursa kwa Taifa Stars

Msimamo wa kundi H kwa sasa unaonyesha kuwa DR Congo wanaongoza kundi hilo wakiwa na pointi tatu baada ya ushindi wao dhidi ya Guinea, huku Tanzania na Ethiopia wakiwa na pointi moja kila mmoja baada ya kutoka sare. Guinea, ambao wanashika nafasi ya mwisho bila alama, wanatarajia kupambana kufa au kupona dhidi ya Taifa Stars ili kujiweka kwenye nafasi bora ya kufuzu kwa AFCON 2025.

Kwa Taifa Stars, ushindi katika mchezo huu utaimarisha nafasi yao katika kinyang’anyiro cha kufuzu na kuwapa motisha zaidi kuelekea michezo ijayo. Stars wameonyesha uwezo mkubwa wa kushindana na timu za viwango vya juu barani Afrika, na safari yao kuelekea Ivory Coast inatarajiwa kuwa hatua muhimu katika safari ya kuelekea Fainali za AFCON 2025.

Mapendekezo  ya Mhariri:

  1. Yanga Kuvaana na CBE Sept 14, Gamondi Aanza Maandalizi Mapema
  2. Kocha Paul Nkata Ajipanga Upya Baada ya Mwanzo Mbaya Ligi Kuu
  3. Simba yaeka Marengo Ya CAF, Mo Dewji Arejea Kuongoza Mikakati
  4. Yanga yazipiku Al Ahly na Sundowns katika Rekodi za Ulinzi
  5. Djuma Shabani atimkia Ufaransa
Nina uzoefu wa miaka zaidi 6 katika uandishi wa habari nchini Tanzania. Shauku yangu ni kuleta habari muhimu katika nyanja mbalimbali ikiwemo Elimu na Michezo