Sowah Aweka Bayana Nia Yake Yakubeba Kiatu Cha Dhahabu
Mshambuliaji mpya wa Singida Black Stars, Jonathan Sowah, ameweka wazi dhamira yake ya kutikisa Ligi Kuu Tanzania Bara kwa ushindani mkali katika mbio za kuwania Kiatu cha Dhahabu msimu wa 2024/2025. Nyota huyo raia wa Ghana amekuwa kwenye kiwango bora tangu ajiunge na Singida Black Stars, akionesha uwezo wa hali ya juu katika safu ya ushambuliaji.
Sowah alijiunga na Singida Black Stars katika dirisha dogo la usajili la Januari 2024 akitokea Al-Nasr Benghazi ya Libya, timu aliyoitumikia kwa miezi sita. Akiwa na kikosi hicho cha Libya, alihusika katika mabao saba kwa kufunga matano na kutoa pasi mbili za mabao katika mechi tisa. Kabla ya kuhamia Al-Nasr Benghazi, Sowah alikuwa akikipiga katika klabu ya Medeama ya Ghana, ambako alionesha kiwango cha juu kwa kufunga mabao 16 katika mechi 20 za Ligi Kuu ya Ghana.
Katika michuano ya Ligi ya Mabingwa Afrika, Sowah alifunga mabao matatu katika mechi saba, jambo lililozifanya klabu mbalimbali kuvutiwa naye, ikiwemo Yanga SC, baada ya kuonesha makali yake dhidi ya miamba hiyo ya Tanzania. Aidha, mchango wake ulisaidia Medeama kutwaa taji la FA nchini Ghana, huku akitwaa tuzo ya Mchezaji Bora wa Mwaka wa timu hiyo na kuorodheshwa kwenye kikosi cha mwisho cha Ghana kilichoshiriki AFCON 2023.
Mafanikio Yake na Singida Black Stars
Tangu ajiunga na Singida Black Stars, Sowah amecheza mechi sita za Ligi Kuu Tanzania Bara na kufunga mabao saba, ikiwa ni wastani wa bao moja kila mchezo. Uwezo wake wa kufumania nyavu umechangia kuleta ushindani mkali katika vita ya ufungaji bora, huku akizidiwa mabao manne na vinara wa orodha hiyo—Jean Charles Ahoua wa Simba SC, Prince Dube na Clement Mzize wa Yanga SC, ambao wana mabao 10 kila mmoja.
Kaimu kocha mkuu wa Singida Black Stars, David Ouma, ameeleza kuwa ujio wa Sowah umeongeza morali kwa washambuliaji wengine wa timu hiyo, hali inayoboresha ushindani ndani ya kikosi. “Malengo yetu ni kumaliza nafasi nne za juu, na hilo linawezekana iwapo kila mchezaji ataendelea kupambana. Sowah ni mshambuliaji mzuri na mchango wake kwa timu ni wa thamani kubwa,” alisema Ouma.
Sowah Azungumzia Malengo Yake
Akizungumzia ushindani wa Kiatu cha Dhahabu, Sowah amesema hana muda wa kupoteza na dhamira yake ni kuhakikisha anakuwa miongoni mwa wafungaji bora wa ligi. “Nilipofika Tanzania, nilitazama msimamo wa wafungaji na nikamwona Elvis Rupia akiwa kinara. Sasa Jean Charles Ahoua wa Simba anaongoza, lakini mimi sijaja kuwa mshabiki, nimekuja kupambana,” alisema mshambuliaji huyo mwenye ari kubwa.
Kwa sasa, msimamo wa wafungaji unaongozwa na Jean Charles Ahoua mwenye mabao 12, akifuatiwa na Clement Mzize na Prince Dube wa Yanga wenye mabao 10 kila mmoja. Steven Mukwala wa Simba na Elvis Rupia wanashikilia nafasi ya tatu wakiwa na mabao tisa, huku Leonel Ateba (Simba) na Peter Lwasa wakiwa na mabao nane. Sowah, pamoja na Stephane Aziz Ki wa Yanga, wanashikilia nafasi ya tano kwa mabao saba kila mmoja.
Mapendekezo ya Mhariri:
- Majeraha ya Goti Yamkosesha Alphonso Davies Mechi za Mwisho za Msimu
- Yanga Yavamia Dili la Fei Simba
- Silaha 6 Muhimu za Simba SC Zatangulizwa Misri
- Vita ya Top 4 Ligi Kuu Tanzania Bara Yapamba Moto
- Morocco Yaishushia Tanzania Kichapo cha 2-0, Mechi ya Kufuzu Kombe la Dunia 2026
- Safari ya Serengeti Boys Kuelekea Kombe la Dunia Yaanzia Morocco
- Kocha Taoussi Akiri Azam FC Kupitia Kipindi Kigumu, Ataka Utulivu
- Matokeo ya Morocco vs Tanzania Taifa Stars Leo 25/03/2025
Leave a Reply