Azam FC Yaichapa KMC 4-0, Taoussi Aanza Kugawa Dozi

Azam FC Yaichapa KMC 4-0, Taoussi Aanza Kugawa Dozi

Katika mchezo wa Ligi Kuu Bara uliochezwa Alhamisi hii, Azam FC ilipata ushindi mnono wa mabao 4-0 dhidi ya KMC FC, ushindi uliomfanya kocha mpya wa Azam, Rachid Taoussi, kuanza kwa kishindo. Mchezo huu uliokuwa wa kwanza kwa Taoussi tangu ajiunge na timu hiyo kutoka Morocco, umerejesha matumaini ya mashabiki wa Azam baada ya mechi tatu mfululizo bila ushindi.

Azam FC, ikiwa ugenini kwenye uwanja wa KMC Complex, ilionyesha kiwango cha juu kwa kumiliki mpira kutoka mwanzo hadi mwisho wa mchezo. Kiungo mahiri Feisal Salum, maarufu kama ‘Fei Toto’, aling’ara kwa kutoa pasi za mabao mawili na pia kuhusika katika bao la nne lililojifungwa na beki wa KMC, Fredy Tangalo, katika harakati za kuokoa mpira mbele ya mshambuliaji wa Azam, Nathaniel Chilambo.

Azam ilianza kuandika karamu ya mabao dakika ya 19, baada ya Fei Toto kumwibia mpira beki wa KMC na kumpasia Idd Seleman ‘Nado’, ambaye alifunga kwa ustadi akimpiga chenga kipa wa KMC, Fabien Mutombora. Bao hilo lilidumu hadi mapumziko licha ya KMC kufanya juhudi za kulisawazisha.

Kipindi cha pili kilianza kwa kasi, na dakika ya 55 nahodha wa Azam, Lusajo Mwaikenda, alifunga bao la pili baada ya kumalizia kazi nzuri ya Fei Toto. Dakika tano baadaye, Nassor Saadun aliongeza bao la tatu, akiwapiga chenga mabeki watatu wa KMC na pia kipa Mutombora, na kuuweka mpira wavuni kwa ustadi mkubwa.

Bao la nne la Azam lilikuja dakika ya 67 baada ya Fei Salum kuambaa pembeni mwa uwanja na kupiga krosi iliyookolewa vibaya na mabeki wa KMC, kabla ya beki Fredy Tangalo kujifunga kwa bahati mbaya.

Azam FC Yaichapa KMC 4-0, Taoussi Aanza Kugawa Dozi

Taoussi Aleta Mabadiliko

Kocha mpya wa Azam FC, Rachid Taoussi, ameonekana kuleta mabadiliko makubwa katika safu ya uchezaji ya timu hiyo. Azam imekuwa ikisuasua katika mechi zilizopita, lakini chini ya uongozi wake, wachezaji wameonyesha mpangilio mzuri wa mashambulizi na utulivu katika safu ya ulinzi. Ushindi huu wa mabao 4-0 siyo tu umeipandisha Azam hadi nafasi ya sita kwenye msimamo wa ligi, bali pia umewapa wachezaji na mashabiki matumaini mapya kwa msimu huu wa 2024/2025.

Rekodi ya KMC Dhidi ya Azam

Kwa upande wa KMC, imeendelea kuwa na historia mbaya dhidi ya Azam FC. Msimu uliopita, KMC ilipoteza kwa mabao 5-0 dhidi ya Azam, na katika rekodi za jumla tangu KMC ilipopanda daraja mwaka 2018, imepoteza mechi nane kati ya mechi 13 dhidi ya Azam. Ushindi wa KMC dhidi ya Azam ni wa mara chache, na mara nyingi wamekuwa wakishindwa katika mechi za ligi.

Matokeo ya Hivi Karibuni Kati ya KMC na Azam

  • 2024/2025: KMC 0-4 Azam
  • 2023/2024: KMC 1-2 Azam | Azam 5-0 KMC
  • 2022/2023: KMC 2-1 Azam | Azam 1-0 KMC
  • 2021/2022: KMC 2-1 Azam | Azam 2-1 KMC
  • 2020/2021: KMC 1-0 Azam | Azam 2-1 KMC
  • 2019/2020: KMC 0-1 Azam | Azam 3-1 KMC
  • 2018/2019: KMC 2-2 Azam | Azam 0-0 KMC

Mapendekezo ya Mhariri:

  1. Wataalam wa Soka Wachambua Utofauti wa Dube na Baleke
  2. Tanzania Ipo Nafasi ya Ngapi Viwango vya FIFA 2024
  3. Viwango vya FIFA Afrika 2024 Timu za Taifa
  4. Kikosi cha Al Ahli Tripoli Chawasili na Bodyguards Kibao Airport
Nina uzoefu wa miaka zaidi 6 katika uandishi wa habari nchini Tanzania. Shauku yangu ni kuleta habari muhimu katika nyanja mbalimbali ikiwemo Elimu na Michezo